Header Ads

Zifahamu dalili,visababishi, aina ,na namna ya kutibu ugonjwa wa kisukari

Je unafahamu mini kuhusu ugonjwa wa kisukari

Ugonjwa wa kisukari au Diabetes Mellitus hutokea pale tezi kongosho au pancrease inaposhindwa kutengeneza homoni au kichocheo aina ya Insulin, au pale mwili unaposhindwa kutumia vizuri kichocheo hicho cha insulin na kusababisha kuongezeka kiwango cha sukari kwenye damu au  kitaalamu hyperglycemia.

Miongoni mwa magonjwa sugu yanayoendelea kuathiri afya za mamilioni ya watu katika nchi nyingi duniani zikiwemo za bara la Afrika na Tanzania ikiwemo ni ugonjwa wa kisukari.

Inakadiriwa kuwa zaidi ya watu milioni 285 wanasumbuliwa na ugonjwa wa kisukari duniani ambapo karibu asilimia 90 ya wagonjwa hao wana aina ya pili ya kisukari. Jambo la kusikitisha zaidi ni kuwa, idadi ya watu wenye kisukari inaongezeka kwa kasi na wataalamu wanasema kuwa, ifikapo mwaka 2030 idadi hiyo itaongezeka maradufu.

Katika miaka ya hivi karibuni kumekuwa na ongezeko la wagonjwa wa kisukari katika nchi za Asia na Afrika, na inasemekana idadi hiyo inatokana na kukua miji na mabadiliko ya maisha ya watu katika nchi zinazoendelea, na labda kutokana na kuiga mifumo ya maisha ya Kimagharibi.

Katika miaka 20 iliyopita wagonjwa wa kisukari wameongezeka kwa kiasi kikubwa nchini Marekani ambapo mwaka 2010 watu milioni 26 walikuwa na ugonjwa huo, huku wengine milioni 7 wakiwa hawajagunduliwa.

Ugonjwa wa kisukari unaweza kusababishwa kuwa na kiwango kidogo cha Insulin mwilini, mwili kutosikia kichocheo hicho au yote mawili. Ili kuelewa vyema ugonjwa wa kisukari ni muhimu kwanza kuelewa namna chakula kinavyovunjwa vunjwa na kutumiwa na mwili ili kuzalisha nguvu.

Wakati chakula kinapoyeyushwa matukio kadhaa hutokea. Moja ni sukari inayoitwa glucose ambayo ni chanzo cha nguvu mwilini huingia katika damu.

Tukio la pili ni kiungo kinachoitwa kongosho au kwa kimombo pancrease kutengeneza kichocheo cha Insulin. Kazi ya Insulin ni kuondoa glucosei katika damu na kuingiza katika misuli, seli za mafuta na ini, ambako hutumiwa kama nishati.

Watu wenye ugonjwa wa kisukari huwa na kiwango kikubwa cha sukari kwenye damu kwa sababu miili yao haiwezi kupeleka sukari kwenye seli za mafuta, ini na misuli ili ihifadhiwe kwa ajili ya kuzalisha nguvu.

Hii ni kutokana na moja ya sababu zifuatazo. Huenda kongosho zao haziwezi kutengeneza insulin ya kutosha, au seli za mwili wao haziathiriwi na insulin kama inavyotakiwa au sababu zote hizo mbili.

UGONJWA WA KISUKARI UMEGAWANYIKA KATIKA MAFUNGU MATATU.

Fungu la kwanza ni Kisukari Aina ya Kwanza au Type 1 Diabetes Mellitus.Hii ni aina ya kisukari inayowaathiri zaidi watoto na vijana. Aina hii hutokea iwapo seli maalumu zinazotengeneza homoni ya insulin zinapokosekana katika tezi kongosho au zinapoharibika kutokana na sababu yeyote ile, na hivyo kusababisha ukosefu kabisa au upungufu wa kichocheo hicho kwenye damu.Mambo yanayoweza kusababisha uharibifu wa seli hizi katika tezi kongosho ni pamoja na kushambuliwa tezi kongosho kunakoweza kufanywa na magonjwa ya kinga ya mwili ya mtu mwenyewe au autoimmune diseases, au kushambuliwa na vyanzo visivyojulikana.

Kwa vile, uharibifu katika tezi kongosho hupelekea kutokuwepo kabisa insulin mwilini au insulin kuzalishwa kwa kiwango kidogo sana, wagonjwa wa aina hii ya kisukari huhitaji kupewa dawa za insulin kwa njia ya sindano au pampu kila siku za maisha yao ili waweze kuishi.
Kwa sababu hiyo aina hii ya kisukari huitwa pia Kisukari kinachotegemea Insulin au Insulin Dependent Diabetes Mellitus (IDDM).

Fungu la pili ni Kisukari Aina ya Pili au Type 2 Diabetes Mellitus.

Hii ni aina ya kisukari inayotokea zaidi ukubwani. Aina hii ya kisukari husababishwa na kupungua utendaji kazi wa homoni ya insulin, au seli kushindwa kutumia insulin ipasavyo.Hali hii mara nyingi husababishwa na unene uliopitiliza yaani obesity, au hali ya kutoushughulisha kabisa mwili (physical inactivity).Kwa vile, katika aina hii ya kisukari, insulin huzalishwa kwa kiwango cha kutosha isipokuwa tatizo lipo kwenye ufanisi na utendaji kazi wake, wagonjwa wa aina hii ya kisukari hawahitaji kupewa insulin kwa njia ya sindano.Ndiyo maana aina hii hujulikana pia kama kisukari kisichotegemea insulin au Non Insulin Dependent Diabetes Mellitus (NIDDM).

Aina ya tatu ya Kisukari ni Kisukari cha Ujauzito auGestationalDiabetes Mellitus.
Ni aina ya kisukari kinachotokea pindi kunapokuwa na ongezeko la kiwango cha sukari katika damu (hyperglycemia) wakati wa ujauzito. Aina hii ya kisukari huathiri karibu asilimia 2 hadi 5 ya mama wajawazito wote ingawa wengi wao hupata nafuu na kupona kabisa mara tu baada ya kujifungua.
Hata hivyo karibu asilimia 20 mpaka 50 ya mama wajawazito wanaopata aina hii ya kisukari huweza kuendelea kuwa na ugonjwa huo hata baada ya ujauzito na hatimaye kuwa na aina ya pili ya kisukari maishani.

KISUKARI HUSABABISHWA NA NINI.

Sababu za kisukari hutofautiana kulingana na aina ya ugonjwa huo.Kwanza tutatuzungumzia yanayosababisha mtu apatwe na aina ya kwanza ya kisukari.Aina ya kwanza ya kisukari ina uhusiano mkubwa sana na kurithi. Aidha aina hii pia husababishwa na maambukizi virusi kama vile Coxsackie virus type B4.Visababishi vingine ni pamoja na sumu inayotokana na kemikali za baadhi ya vyakula (food borne chemical toxins), na kwa baadhi ya watoto wachanga maziwa ya ng’ombe yanaweza kuchochea kinga ya mwili wa mtoto uushambulie mwili wenyewe na hivyo kusababisha uharibifu katika tezi kongosho.

Aina ya pili ya kisukari kwa ujumla husababishwa zaidi na jinsi mtu anavyoishi na pia matatizo ya kijeneteki. Aidha kuongezeka uzito na unene kupita kiasi (obesity) vilevile huchangia kutokea aina hii ya kisukari.

Sababu nyingine ni pamoja na kuongezeka umri, maisha ya kivivu na kutofanya mazoezi na pia ugonjwa wa tezi kongosho (pancreatitis) ambao hufanya insulin inayozalishwa kuwa na ufanisi mbovu au ya kiwango cha chini.

DALILI ZA UGONJWA WA KISUKARI NI ZIPI?
DALILI HIZO NI:

Kukojoa mara kwa mara hali inayojulikana kitaalamu kama polyuria.Mgonjwa kuhisi kiu kali na kunywa maji kwa kiwango cha kupitiliza (polydipsia).Mgonjwa kuhisi njaa na kula mara kwa mara (polyphagia).Kuchoka haraka Kupungua uzito Vipele mwilini ambavyo kitaalamu huitwa diabetic dermadromes.

Na wagonjwa wa kisukari pia huwa katika hatari ya kupata maambukizi katika kibofu cha mkojo, ngozi na kwa wanawake sehemu za siri.

Aidha kuna dalili maalumu ambazo hutokea kwa wagonjwa wa kisukari iwapo mgonjwa atapatwa na mojawapo ya madhara (complications) ya ugonjwa huo.

Madhara hayo ambayo hujulikana kwa kifupi DKA hutokea kwenye aina ya kwanza ya kisukari na huwa na dalili zifuatazo

Mgonjwa kutoa harufu ya acetone (inayofanana kidogo na harufu ya pombe).Mgonjwa hupumua kwa haraka na kwa nguvu,kujihisi kichefuchefu,kutapika,kuhisi maumivu ya tumbo na kupoteza fahamu.Kupoteza fahamu mgonjwa kunakoitwa Hyperosmolar Non-ketotic coma hutokea kwenye kisukari cha aina ya pili ambapo mara nyingi husababishwa na upungufu wa maji mwilini.

Baada ya mtu kuwa na dalili za ugonjwa wa kisukari matibabu huanza baada ya kufanyiwa vipimo na kuthibitisha kwamba kweli ana ugonjwa huo.

Baada ya vipimo tunaweza kusema mtu fulani ana kisukari iwapo:
1) Kiwango cha sukari kwenye damu kinatakuwa sawa na 126mg/L, kipimo ambacho kwa kawaida hufanyika kwa mtu ambaye hajakula chakula chochote. Kwa jina jingine kipimo hiki huitwa Fasting Blood Glucose (FBG).

2) Kiwango cha sukari kwenye damu kinapokuwa sawa na 200mg/L kwa mtu ambaye amelishwa gram 75 za glucose ndani ya masaa mawili. Kipimo hiki pia huitwa Oral Glucose Tolerance Test (OGTT). Au iwapo mgonjwa atafanyiwa kipimo kinachoitwa glycoslytated hemoglobin (Hb A1C) na kuwa chanya

KISUKARI HUWEZA KUSABABISHA MADHARA YAFUATAYO KWA MHUSIKA IWAPO HAKITATIBIWA INAVYOPASWA.

Kuziba kwa mishipa mikubwa ya damu kutokana na kuzungukwa na mafuta (Atherosclerosis).Mgonjwa kushindwa kuona vizuri au kushindwa kuona kabisa na kuwa kipofu (diabetic retinopathy)Kushindwa kufanya kazi vizuri kwa figo,Mgonjwa kuhisi ganzi na kupoteza hisia mikononi na miguuni kwa sababu ya kuharibika kwa neva (diabetic neuropathy),Kupungua kwa nguvu za kiume.Vidonda (diabetic ulcers) hususan vidoleni.

Hali hii wakati mwingine humpelekea mgonjwa kukatwa viungo vyake.
Mgonjwa kuwa katika hatari ya kupata maambukizi ya vimelea mbalimbali hasa bakteria kutokana na kuharibika na kushindwa kufanya kazi vizuri kwa chembe nyeupe za damu.

Ugonjwa wa kisukari kama hautodhibitiwa unaweza kumsababishia mgonjwa madhara makubwa na kuathiri karibu kila kiungo mwilini.

Kama tulivyosema ugonjwa huo huathiri moyo na mishipa ya damu, macho, figo neva na hata fizi na meno. Ingawa mgonjwa wa kisukari anapotibiwa na kujua jinsi ya kudhibiti kiwango chake cha sukari mwilini suala hilo hupunguza na kuzuia madhara ya ugonjwa huo, lakini kwa bahati mbaya hata kisukari kinachodhibitiwa vyema baada ya muda mrefu humuathiri mgonjwa.

Takwimu zinaonyesha kuwa, wagonjwa wenye kisukari hufa zaidi ikilinganishwa na wasiokuwa na ugonjwa huo kutokana na madhara wanayoyapata, sababu kuu ikiwa ni ugonjwa wa moyo.

Zaidi ya asilimia 60 ya wagonjwa wa kisukari hupata mshituko wa moyo huku asilimia 25 wakipata kiharusi.

Njia bora zaidi ya kuzuia hayo yote ni kuhakikisha kwamba kiwango cha glucose katika damu kiko katika hali yake inayotakiwa kila wakati, suala ambalo kwa bahati mbaya huwa gumu kwa wenye ugonjwa huo.

Watu wazima wenye ugonjwa wa kisukari hushambuliwa na maradhi ya moyo mara mbili hadi 4 zaidi kuliko wasiokuwa na ugonjwa huo, na hatari ya kupata mshituko wa moyo ni mara 4 zaidi kwa wagonjwa hao.
Tafiti pia zinaonyesha kwamba, kuharibika mishipa ya damu au kuharibika neva kunaweza kusababisha matatizo ya miguu kwa wagonjwa wenye kisukari, suala ambalo huenda likapelekea kukatwa miguu.

Utafiti unaeleza kuwa zaidi ya asilimia 60 ya miguu inayokatwa bila kuumia sababu kuu huwa ni kisukari. Nchini Marekani ugonjwa huo ni chanzo kikuu cha watu wenye umri kati ya miaka 20 hadi 74 kuwa vipofu. Inasemekana kuwa, hata kama mgonjwa wa kisukari atatibiwa na kudhibiti vyema kiwango cha sukari mwilini, lakini baada ya miaka kadhaa taratibu ugonjwa huo huathiri macho na moyo wake. Kwa wale ambao hawajali matibabu na kudhibiti kiwango cha glucose mwilini hupata madhara hayo mapema zaidi.

Baada ya kuyaona madhara ya kisukari kwa viungo kadhaa mwilini, suala hilo linatuonyesha umuhimu wa kujikinga na ugonjwa huo na pia umuhimu wa kuutibu na kuudhibiti kwa wale ambao tayari ni wagonjwa.

Matibabu ya kisukari hutegemea aina ya kisukari ingawa kwa ujumla hujumuisha matumizi ya dawa na njia ya kubadilisha mfumo au staili ya maisha. Kwa aina ya pili ya kisukari au Type 2 DM, aina hii ya kisukari huweza kutibiwa ama kwa dawa, kubadili mfumo wa maisha au vyote viwili kwa pamoja.

Katika kubadili mfumo wa maisha, ni muhimu mgonjwa kutilia maanani na kuwa makini na aina ya vyakula anavyokula na kujitahidi kufanya mazoezi na kuushughulisha mwili ili kuepuka kuongezeka uzito kupita kiasi. Kuhusiana na aina ya vyakula inashauriwa sana.

Kupunguza kula vyakula vyenye mafuta ya kolestroli ambayo ni mafuta mabaya, yaani kula walau chini ya miligramu 300 za kolostroli kwa siku.Kujitahidi sana kula vyakula vya kujenga mwili vya proteini angalau kwa asilimia 10-15 kwa siku. Vyakula hivi ni pamoja na nyama na mboga za majani.Kuwa makini na ulaji wa vyakula vya wanga au carbohydrate. Inapasa kuhakikisha kuwa havizidi asilimia 50-60 ya chakula unachokula kwa siku na visiwe ndicho chakula kikuu kwa siku.Kupunguza utumiaji wa chumvi katika chakula na kuacha kabisa au kupunguza kunywa pombe.

Suala la ufanyaji mazoezi ni jambo muhimu kwa vile mazoezi husaidia sana kupunguza uzito, kuondoa mafuta yanayopunguza utendaji kazi wa Insulin mwilini na hivyo kuongeza ufanisi na utendaji wa homoni hiyo muhimu mwilini.

Vilevile mgonjwa mwenye aina hii ya kisukari anaweza pia kupewa dawa ambazo atatakiwa kunywa kila siku huku akiendelea kufuata ushauri kama tulivyoeleza.
Dawa hizo ambazo huitwa pia dawa za kushusha kiwango cha sukari mwilini (Oral Hypoglycemic drugs) ni kama vile Metformin na Glipizide.

Ifahamike pia kuwa, wapo baadhi ya wagonjwa wa aina hii ya pili ya kisukari (Type 2 DM) ambao pamoja na kutumia dawa za kunywa za kushusha sukari na kufuata ushauri wa daktari kuhusu mfumo wao wa maisha bado njia hizo zinaweza zisishushe sukari inavyotakiwa. Katika hali kama hiyo, wagonjwa hawa huweza pia kudungwa sindano za Insulin kwa muda ili kushusha kiwango cha sukari mwilini.

Katika matibabu ya Aina ya Kwanza ya kisukari au Type 1 DM pamoja na kurekebisha aina ya vyakula na kufanya mazoezi, wagonjwa huhitaji kichocheo cha Insulin ili kudhibiti kiwango cha sukari katika damu.

DAWA ZA INSULIN ZIMEGAWANYIKA KATIKA MAKUNDI MAKUU MATATU.
Kuna zile zinazofanya kazi kwa muda mfupi, za muda wa kati na zinazofanya kazi kwa muda mrefu.
Kulingana na utendaji wa dawa hizo, mgonjwa anaweza kuelekezwa jinsi ya kujidunga mwenyewe sindano za Insulin nyumbani kwa kufuata maelekezo yafuatayo:

Asubuhi: Mgonjwa hujidunga 2/3 ya insulin nusu saa kabla ya kunywa chai.
Usiku: Mgonjwa hujidunga 1/3 ya insulin nusu saa kabla ya chakula cha usiku.

Aidha katika hii 2/3 inayotolewa asubuhi, 2/3 yake huwa insulin inayofanya kazi kwa muda wa kati na 1/3 ni ile inayofanya kazi haraka au kwa muda mfupi.

KUMBUKA

Inasisitizwa sana kutojidunga sindano za ugonjwa huo bila kupata maelekezo sahihi ya daktari. Kwa maelekezo zaidi na sahihi ya matibabu kwa kutumia Insulin ni vizuri kuhudhuria kiliniki za kisukari.Pia njia za kutibu ugonjwa wa sukari hutolewa hospitalini, na hayo ni matibabu maalumu yakoma aina ya hyperosmolar non-ketotic (HONKC).Mkazo huwekwa katika kusahihisha upungufu wa maji mwilini ambapo mgonjwa hupewa kati ya lita 8 hadi 10 za maji aina ya Normal saline.Iwapo kuna ugumu katika kusahihisha kiwango cha sukari mwilini kwa kutumia dawa za kunywa, Insulin inaweza kutolewa. Matibabu mengine maalumu ni ya kutibu Diabetic Ketoacidosis(DKA).Kama ilivyo kwa hyperosmolar non-ketotic coma, matibabu ya DKA nayo hutolewa hospitali chini ya uangalizi maalumu wa madaktari. Hii ni hali ya hatari, ambapo isipotibiwa kwa umakini, inaweza kumuua mgonjwa.Jambo la muhimu katika matibabu haya ni kusahihisha upungufu wa maji mwilini, kusahihisha kiwango cha potassium katika damu na kurekebisha kiwango cha sukari kwenye damu kwa kutumia Insulin.

Wasomaji wa Blog hii na makala hii
tunapaswa kujua kuwa unene na kuongezeka uzito wa mwili kwa kiwango cha kupindukia ni miongoni mwa sababu kuu zinazopelekea mtu kupata magonjwa mbalimbali kama vile ugonjwa wa moyo, kiharusi, kisukari, shinikizo la damu na mengineyo.

Pia baadhi ya tabia kama vile kuvuta sigara, kunywa pombe, kutumia madawa ya kulevya na ngono za ovyo vile vile husababisha mtu kupatwa na baadhi ya maradhi.

Kwa kuwa suala la unene wa kupita kiasi limekuwa janga la kiafya katika nchi nyingi hasa zinazoendelea na ni suala nyeti ambalo humsababishia mtu magonjwa mbalimbali kikiwemo kisukari.

Namalizia kwa utafiti unaosema kwamba, wale
wanaokoroma wakati wakilala, wanakabiliwa na hatari kubwa ya kupatwa na ugonjwa wa kisukari kuliko wale wanaolala kimya. Kwa mujibu wa uchunguzi huo uliofanywa kwenye chuo kikuu cha Yale nchini Marekani,

Wale wanaokoroma sana wanapolala,
wanakabiliwa na hatari ya kupata kisukari kwa asilimia 50. Wataalamu wanasema pia kuwa, kushindwa kupumua usingizini huenda kukahusiana na kisukari aina ya pili, bila kujali sababu nyinginezo kama vile umri, jinsia, uzito na hata asili anayotoka mtu.

Kukoroma sugu, au kitaalamu sleep apnea ni hali inayosababishwa na kushindwa kufanya kazi njia ya hewa, suala ambalo humfanya mtu aamke mara kadhaa usingizini wakati anapolala.

Hali hiyo inahusiana na baadhi ya mabadiliko ya umetaboli au hali ya ujenzi wa seli na uvunjaji vunjaji wa kamikali zinatokana na chakula mwilini, kwa kimombo ‘metabolism’

No comments

Powered by Blogger.