Header Ads

WAKULIMA KOROSHO WAPINGA AKAUNTI

Haya yanatokea siku chache baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kumaliza ziara ya kikazi wilayani Ruangwa. Wengi hawaafiki.

Wakulima kadhaa kutoka kata za Chenjele, Luchelegwa, Mandawa, Namichiga, Chunyu na Matambarale ambako Majaliwa amepita na wameiambia Nipashe kwa simu jana kuwa, hawaelewi watakavyouza korosho zao kwa sababu hawana akaunti benki na wengi wao wana korosho chache kati ya debe moja na sita.

Juma Ngulamba mkulima kutoka Chenjele alisema anapata shinda kuona ana debe tatu za korosho msimu huu lakini ameambiwa hawezi kuuza hadi awe na akaunti benki.

Zaituni Mwambe mkazi wa kijiji cha Luchelegwa alisema hawezi kufungua akaunti benki kwa ajili ya kupokelea fedha za debe mbili kisha akaunti ikabaki haina kazi wakati wote.

Sophia Malibiche kutoka katika Kijiji cha Nandandara kata ya Matambarale alisema, ana gunia moja msimu huu, lakini ameambiwa hawezi kuuza hadi awe na akaunti benki, jambo ambalo anakiri kuwa limemvuruga akili.

"Ukipima gunia langu moja la korosho lenye kilo kati ya 70 na 80 utapata Shilingi 92,000 ambazo pia unapewa kwa mkopo kwa kulipwa kidogokidogo kwa sababu korosho zimo katika mfumo wa stakabadhi ghalani," alisema.

Alisema vyama vya ushirika vya msingi ngazi ya kata vinapaswa kubuni utaratibu mbadala utakaosaidia wakulima wadogo kuuza korosho zao bila kuwa na akaunti benki kwa sababu utaratibu huo ni mgumu kwa wakulima wadogo.

Kwa upande wake mkulima mwingine mdogo kutoka Kijiji cha Mbuyuni kata ya Namichinga, Sarafina Lijoka, amesema kuwa amevuna debe nne na anatakiwa kuwa na akaunti, hivyo amekata tamaa.

Akuzungumzia hali hiyo kwa simu kutoka Liwale, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika kinachounganisha Wilaya za Ruangwa, Nachingwea na Liwale mkoani Lindi (RUNALI), Hassan Mpako, alikiri kuwapo kwa hofu miongoni mwa wakulima wadogo, lakini akasema jambo hilo litapatiwa ufumbuzi.

"Wakati wa ziara Waziri Mkuu aliambiwa juu ya jambo hilo na ameshatoa maelekezo ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi bila shaka hadi kesho mnada wa kwanza wa korosho unapofanyika mjini Nachingwea, tutakuwa tumepata majibu," alisema Mpako.

No comments

Powered by Blogger.